UMOJA wa Mataifa umethibitisha kuwa umepata kibali kutoka kwa Serikali ya Israel kuruhusu malori takribani 100 yaliyojaa misaada ya kibinadamu kuingia katika Ukanda wa Gaza.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi, Msemaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu (OCHA), Jens Laerke, amesema kuwa kibali hicho kinatoa nafasi kwa shehena kubwa ya misaada kuwasilishwa kwa wakazi wa Gaza ambao wanakabiliwa na hali mbaya ya kibinadamu.
“Tuliwasilisha ombi la kuingiza malori mengi zaidi ya yale yaliyoidhinishwa awali, na tumepata idhini hiyo. Tunatarajia kwamba ifikapo leo (Jumatano), malori hayo yatachunguzwa na kuruhusiwa kuvuka hadi kufika maeneo ya ndani ya Gaza kwa ajili ya kusambaza misaada,” alisema Laerke.
