Kundi la Hamas limesema mateka wa mwisho raia wa Marekani Edan Alexander, ataachiliwa huru kama sehemu ya juhudi za kusitisha mapigano, kufungua tena njia za kuingia Gaza na kuwezesha usambazaji wa misaada ya kibinadamu.
Maafisa wawili wa Hamas wameliambia shirika la Habari la Associated Press kwamba wanatarajia kumuachilia huru mateka huyo katika muda wa saa 48 zijazo.
Mjumbe wa Rais wa Marekani Donald Trump wa eneo la Mashariki ya Kati Steve Witkoff, amethibitisha jana hilo Mei 11, 2025 kuwa Hamas imekubali kumuachilia Alexander kama ishara ya nia njema kuelekea kwa kiongozi huyo wa Marekani.
Tangazo la kuachiliwa kwa mateka huyo kwa mara ya kwanza tangu Israel ilipokiuka mpango wa usitishaji mapigano mnamo mwezi Machi, limetolewa muda mfupi kabla ya Trump kufanya ziara Mashariki ya Kati wiki hii.