Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa anatarajia kukutana na Rais wa Marekani Donald Trump wiki ijayo nchini Marekani katika ziara rasmi.
Katika taarifa afisi ya Ramaphosa imesema Rais huyo atakutana na Trump katika ikulu ya White House wakati ambao mahusiano kati ya Marekani na Afrika Kusini yakiwa yameingia doa tangu Donald Trump arudi madarakani mwezi Januari.
Trump amekata misaada yote ya kifedha ya Marekani kwa Afrika Kusini, akikosoa sera yake ya mageuzi ya umiliki wa ardhi na kesi ya mauaji ya halaiki ambayo Afrika Kusini iliiwasilisha katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC dhidi ya Israel, nchi ambayo ni mwandani wa Marekani.
Wiki hii utawala wa Trump uliwakaribisha Marekani, Waafrika Kusini 49 weupe, ukisema wamekuwa wahanga wa ubaguzi wa rangi huko Afrika Kusini huku Serikali ya Afrika Kusini ikikanusha madai ya Trump ikisema hakuna ushahidi wa kuteswa kwa Waafrika Kusini weupe nchini humo.