Baada ya kusambaa kwa uvumi mitandaoni juu ya taarifa za kifo cha Rais Salva Kiir, Serikali ya Sudan Kusini imekanusha imekanusha uvumi huo na kusema kuwa sio kweli.
Kulizuka taarifa katika mitandao ya kijamii hapo juzi kwamba Kiir ameaga Dunia ila wizara ya mambo ya nje ya Sudan Kusini imetoa taarifa jana ikisema, hizo ni taarifa za uongo.
Kiir mwenye umri wa miaka 73, kwa muda mrefu amekuwa akidaiwa kuwa na matatizo ya kiafya ingawa katika miezi ya hivi karibuni, ameonekana akikutana na viongozi wanaoizuru nchi hiyo na hata akiamrisha kufanyika mabadiliko katika Serikali yake.
Haya yanafanyika wakati ambapo nchi hiyo inakabiliwa na kitisho cha kuzuka tena mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, kufuatia makabiliano kati ya vikosi vinavyomuunga mkono Kiir na vile vitiifu kwa makamu wake Riek Machar ambaye Kiir alimuweka katika kifungo cha ndani.