Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ameridhishwa na Maandalizi kuelekea sherehe za siku ya wafanyakazi Duniani zitakazofanyika kesho Mei mosi, 2025 kitaifa Mkoani Singida katika Uwanja wa Bombadia
Ameyasema hayo leo Jumatano Aprili 30, 2025 alipopokea taarifa na kukagua maandalizi ya Maadhimisho ya Sherehe hizo ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Majaliwa ameipongeza kamati inayoratibu sherehe hizo na kuwataka kuhakikisha wanakamilisha maeneo machache yaliyobaki ambayo yanahitaji maboresho.
Awali, akitoa taarifa ya maandalizi hayo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Ridhiwani Kikwete amesema maandalizi yamekamilika kwa kiasi kikubwa na wapo tayari kumpokea Rais Dkt. Samia kwa ajili ya sherehe hizo.